WAZIRI MKUU: WATANZANIA TUNZENI AKIBA YA CHAKULA
..Ahimiza matumizi ya mbolea na mbegu za mazao ya muda mfupi. Na Mwandishi Wetu, Dodoma. WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania watunze akiba ya chakula walichonacho na waepuke matumizi yasiyofaa kutokana na hali ya kuchelewa kwa msimu wa mvua. Waziri Mkuu ametoa wito huo leo jioni (Jumapili, Desemba 14, 2025) wakati akizungumza na baadhi ya Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma. Amewaeleza viongozi hao kutoka mikoa ya Dodoma na Singida kwamba Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitoa utabiri wa mwelekeo wa msimu wa mvua za vuli na mvua za msimu kwa kipindi cha Oktoba 2025 hadi Desemba 2025 na kipindi cha mwezi Novemba, 2025 hadi Aprili 2026 mtawalia. “Kutokana na utabiri huo, baadhi ya mikoa nchini inatarajiwa kuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani na kutawaliwa na vipindi virefu vya ukavu na mtawanyiko wa mvua usioridhisha,” amesema. Amesema tathmini hiyo ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaonesha hali ya...