MJIKO BANIFU KWA BEI YA RUZUKU YAWAFIKIA WANANCHI CHUNYA.
Majiko 1,555 kuuzwa kwa bei ya ruzuku, Serikali kutoa ruzuku ya asilimia 85 kwa kila jiko. Na Mwandishi Wetu, Chunya - Mbeya* KAIMU Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chunya ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa halmashauri hiyo, Wakili Athumani Bamba leo Aprili 24, 2026 amezindua rasmi mradi wa usambazaji na uuzaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku katika mji mdogo wa Makongolosi, wilayani Chunya mkoani Mbeya. Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Kaimu Mkurugenzi huyo alisema mradi huo unalenga kuwapatia wananchi nishati mbadala iliyo nafuu, salama na rafiki kwa mazingira, huku ukichochea kupunguza matumizi makubwa ya kuni na mkaa ambao umeendelea kuwa chanzo cha uharibifu wa misitu. Ameeleza kuwa kupitia mpango huo wa ruzuku, wananchi wataweza kumudu kununua majiko banifu kwa gharama nafuu zaidi, jambo litakalosaidia kupunguza matumizi ya nishati zisizo rafiki pamoja na kuboresha afya za watumiaji kwa kupunguza athari za moshi majumbani. “Ni muhimu wananchi wakautumia vyem...